Serikali imeagizwa kuwarudishia pesa watu wote waliowekwa kwenye vituo vya karantini kwa lazima.
Uamuzi huu umetolewa na jaji wa mahakama kuu James Makau ambaye ameamuru kuwa ilikuwa kinyume cha sheria kwa serikali kuwaweka watu kwenye karantini kwa lazima bila kupata agizo la mahakama inavyotakikana kisheria.
Akitoa uamuzi kwenye kesi iliyowasilishwa mahakamani na mwanaharakati Okiya Omtatah, jaji Makau amesema wizara ya afya ilikiuka haki za wale waliowekwa kwenye vituo hivyo kwa lazima.
Ameamuru kuwa serikali ilikuwa inapaswa kuchukua jukumu la kuwagharamia watu wote waliowekwa kwenye karantini kwa sababu taifa lilikuwa linakabiliana na janga la kimataifa.
Omtatah aliishtaki serikali kufuatia hatua ya kuwaweka watu kwenye karantini kwa lazima na kisha kuwaacha kulipa gharama zote wanapokuwa kwenye vituo hivyo.