Muwaniaji wa chama cha Maendeleo Chap Chap katika uchaguzi mdogo wa useneta katika kaunti ya Machakos amejiondoa kutoka kinyanganyiro hicho.
Kiongozi wa chama hicho Alfred Mutua amesema John Mutua Katuku amekubali kujiondoa kufuatia wito wa Rais Uhuru Kenyatta kuwepo kwa amani na utulivu wakati wa zoezi hilo la hapo kesho.
Tangazo la Mutua limejiri muda mfupi baada ya kikao na Rais Kenyatta ambacho kiliwajumuisha viongozi kutoka vyama vingine vya kisiasa ikiwemo ODM, Wiper Ford Kenya, Narc na Amani National Congress.
Wawaniaji wengine kwenye kinyangiro hicho ni Agnes Kavindu wa chama cha Wiper, Urbanus Ngengele wa United Democratic Alliance party’s (UDA) na John Musingi wa chama cha Muungano.
Wengine ni Stanley Masai Muindi wa chama cha Economic Democracy, Edward Musembi wa Ford Asili, Simeon Kioko Kitheka wa Grand Dream Development na wawaniaji huru Sebastian Nzau, Jonathan Maweu na Francis Musembi.