Rais Uhuru Kenyatta akiwa ameandamana na kinara wa chama cha ODM Raila Odinga ameanza rasmi ziara yake katika eneo la Ukambani kwa kukagua ujenzi wa bwawa la maji la Thwake katika kaunti ya Makueni.
Ujenzi wa bwawa hilo umepewa kipau mbele kwenye mipango ya serikali kuafikia ruwaza ya mwaka 2030.
Katika ziara yake, rais Kenyatta pia amekagua ujenzi wa barabara ya Kibwezi-Kitui itakayounganisha kaunti za Makueni-Machakos na Kitui.
Rais Kenyatta vile vile amekagua mradi wa Konza City ulioko Machakos na unaogharimu mabilioni ya pesa.
Rais alikuwa ameandamana na viongozi kutoka Ukambani wakiongozwa na kinara wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka, magavana Kivutha Kibwana (Makueni) na Charity Ngilu (Kitui).