Rais Uhuru Kenyatta ametia saini mswada wa marekebisho ya sheria za tume ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC.
Marekebisho hayo yanatoa fursa ya kubuniwa kwa jopo ambalo litawatafuta watu watakaojaza nafasi za makamisha wanne wa tume hiyo waliojiuzulu.
Roselyn Akombe alikuwa wa kwanza kujiuzulu siku nane pekee kabla ya marudio ya uchaguzi wa urais tarehe 26 Oktoba mwaka 2017 akidai kuwa tume hiyo ilikuwa imeingiliwa na haingeweza kuandaa uchaguzi huru na wa haki.
Aprili mwaka 2018, makamisha wengine watatu akiwemo naibu mwenyekityi Connie Nkatha Maina, Margaret Mwachanya na Paul Kurgat walijiuzulu na kudai baada ya kudai kuwa hawakuwa na imani na mwenyekiti wao Wafula Chebukati.
Hatua hii pia inaonekana kutengeneza njia ya kuandaliwa kwa kura ya maamuzi kupitia kwa ripoti ya BBI ambayo ilizinduliwa siku ya Jumatatu.