Maseneta wametakiwa kuharakisha mchakato wa kutanzua utata unaozingira mswada wa ugavi wa mapato ili kuziokoa serikali za kaunti.
Waziri wa Ugatuzi Eugene Wamalwa anasema kuendelea kucheleweshwa kwa pesa zinazofaa kupewa kila kaunti kunahujumu shughuli za utoaji huduma hali inayoelezea haja ya utata huo kutatuliwa kwa haraka.
Baraza la magavana likiongozwa na mwenyekiti wake gavana wa Kakamega Wycliffe Oparanya limetishia kuwatuma nyumbani wafanyikazi wake tarehe kumi na saba mwezi huu kwa kushindwa kuwalipa mishahara.
Baraza hilo aidha limetishia kuwa litawasilisha hoja ya kuvunjilia mbali bunge la seneti kwa kukosa kuafikia suluhu la mfumo utakaotumika kugawa shilingi billion 316.