Chama cha mawakili nchini LSK kimetaja kama kinyume cha sheria mchakato wa kumtafuta mrithi wa jaji mkuu David Maraga kabla yake kustaafu Januari mwaka ujao na kuapa kuelekea mahakamani kuupinga.
LSK kupitia rais wake Nelson Havi imesema imeshangazwa na msimamo uliotolewa na mwakilishi wake katika tume ya huduma za mahakama (JSC) Macharia Njeru kuhusu swala hilo na kusisitiza kwamba wadhifa huo unafaa kujazwa baada ya kuondoka kwa Maraga.
Havi amedai kuwa Maraga anasulubishwa kwa kulazimishwa aende kwa likizo ya mapema kwa sababu ya msimamo wake wa kuheshimu sheria ikiwemo kubatilisha uchaguzi wa urais mwaka 2017.
Kauli za LSK zinawadia saa chache baada ya Macharia Njeru ambaye ni mwakilishi wake katika tume ya huduma za mahakama JSC kumtuhumu Maraga kutokana na kile alitaja kama kuhujumu juhudi za kumtafuta mrithi wake kama rais wa mahakama ya upeo.
Njeru anadai kuwa Maraga anamtumia naibu wake Phlomena Mwilu na jaji Mohamed Warsame kuzuia kuanza mchakato huo wa kumrithi.
Maraga anatazamiwa kuelekea kwenye likizo Disemba 15 kabla ya kustaafu kwake Januari 21 mwaka ujao 2021.