Italia, taifa ambalo limeathirika zaidi na virusi vya Corona mbali na China limeripoti maafa ya watu 475 kufikia Jumatano huku ulimwengu ukijitahidi kukabiliana na janga hilo kwa kufunga shule, miji na kuweka sheria kali kwenye mipaka yao.

Uingereza limekuwa taifa la hivi punde kutangaza kuwa itafunga shule wakati ambapo shinikizo zinazidi kuiandama serikali kuchukua hatua.

Marekani na Canada tayari wametangaza hatua za kufunga mipaka yao.

Zaidi ya watu laki mbili wamethibitishwa kuambukizwa virusi hivyo kote duniani,  watu 83, 000 wakipona na wengine 8, 000 wakifariki kwa mujibu wa data kutoka kwa chuo kikuu cha  Johns Hopkins nchini Marekani.

Nchini China ambako mlipuko wa ugonjwa huo ulianzia, mikoa ya Wuhan na Hubei haijaripoti kisa chochote kipya cha maambukizi baada ya kufungwa kwa muda wa miezi miwili.