Mabunge ya kaunti ya Kisii, Vihiga, Laikipia na Nairobi yamekuwa ya hivi punde kupitisha mswada wa marekebisho ya katiba BBI.
Hii inamaanisha kuwa mswada huo sasa unahitaji kuungwa mkono na mabunye ya kaunti 13 zaidi ili kufanikisha hatua inayofuata ya mabadiliko ya sheria.
Kaimu spika wa bunge la kaunti ya Kisii Amos Onderi anasema uamuzi wa kupitisha mswada huo uliafikiwa kwa kauli moja.
Gavana wa kaunti hiyo ya Kisii James Ongwae amelipongeza bunge la kaunti hiyo kwa kupitisha mswada huo.
Katika bunge la kaunti ya Nairobi, kiongozi wa walio wengi Abdi Guyo na mwenzake wa Baba Dogo Geoffrey Majiwa waliwaongoza wenzao kupigia debe mswada huo wakisema Nairobi itanufaika pakubwa iwapo utapistihwa.
Kwa kauli moja madiwani hao wapatao mia moja kumi na wanne walipitisha mswada huo pasipokuwa na anayepinga.
Seneta wa Nairobi Johnson Sakaja, mbunge wa Makadara George Aladwa, mwenzake wa Embakasi Mashariki Babu Owino pamoja na mbunge mteule Maina Kamanda walihudhuria vikao hivyo.
Mabunge ya Kisii, Vihiga, Laikipia na Nairobi yanajiunga na Kajiado, Trans Nzoia, Pokot Magharibi, Busia, Homa Bay, Kisumu na Siaya kupitisha mswada huo.
Bunge la kaunti ya Baringo ndilo la kipekee kupinga mswada huo kufikia sasa.
Mswada huo unahitaji kuungwa mkono na mabunge ya kaunti yapatayo 24 kati ya 47 ili kufanikisha mabadiliko ya sheria.
Wakati uo huo
Baadhi ya madiwani wa kaunti ya Machakos wametishia kuangusha mswada wa BBI iwapo gavana Alfred Mutua hataheshimiwa.
Wakizungumza katika afisi za gavana huyo wawakilishi wadi hao wamesema gavana Mutua ameendelea kudharauliwa licha ya mchango wake katika mchango mzima wa BBI.